Kwa muda mrefu kumekuwa na mjadala mkubwa ikiwa mjasiriamali anazaliwa au anatengenezwa. Kwa kuangalia tabia za wajasiriamali na tabia za binadamu kwa ujumla, wajasiriamali wana tabia za kipekee. Wajasiriamali wanafikiri tofauti na wanatenda tofauti na watu wengine kwenye jamii.
Tabia za kipekee zinazooneshwa na wajasiriamali kuna ambao wamezaliwa nazo na kuna ambao wamezipata kutoka kwenye mazingira na shughuli wanazofanya.
Hapa nitaelezea tabia thelathini(30) ambazo ni dalili tosha kwamba wewe ni mjasiriamali. Kama huna tabia hizi unaweza ukaanza kujifunza taratibu na baadae ukawa na tabia za kijasiriamali. Kumbuka tofauti kubwa ya mjasiriamali ni jinsi anavyofikiri na kuchukua hatua tofauti na watu wengine. Kwa mfano wakati mwajiriwa anaweza kukubaliana na shida anazopata kwenye ajira yake na kuona hakuna anachoweza kufanya, mjasiriamali anafikiria uwezo wa tofauti alionao na jinsi anavyoweza kwenda kuutumia nje ya ajira na akafanikiwa. Baada ya hapo anaweza kuacha kazi na kwenda kufanya lile litakalomridhisha. Kwa kuwa na mtizamo chanya na utayari wa kuchukua hatua kunawafanya wajasiriamali kupata mafanikio makubwa.
Kama unatabia hizi 30, ni dalili tosha kwamba wewe ni mjasiriamali, unatakiwa kuchukua hatua mara moja ili kufikia mafanikio makubwa;
1. Hukubaliani na mfumo. Mara nyingi umekuwa ukihoji kwa nini kitu fulani kifanyike na umekuwa ukijitahidi kutafuta njia bora zaidi ya kufanya kazi fulani pale unapokuwa umeajiriwa. Hufanyi kitu bila ya kuhoji umuhimu wake na kufikiri njia ya kuboresha.
2. Unaonekana kama mfanyakazi mkorofi. Wakati mwingine umeshafukuzwa kazi mara kadhaa kutokana na tabia yako ya kuhoji na kutaka kuboresha utendaji kazi. Au umeshaacha kazi au kupanga kufanya hivyo kutokana na kutoridhishwa na kazi hiyo.
3. Una hamasa kubwa ya kutekeleza majukumu yako. Husubiri upangiwe cha kufanya, unajua majukumu yako na unayafanya kwa ubora wa hali ya juu.
4. Ukiambiwa hapana huridhiki, hapana sio jibu kwako unaendelea kutafuta njia nyingine mpaka upate NDIYO.
5. Unajiamini na unaamini una uwezo mkubwa wa kufanya mambo makubwa. Una uhakika hata kitokee kitu gani bado unauwezo wa kusimama na kuleta tofauti.
6. Ni mtu wa watu, unaweza kuchangamana na watu wa aina zote. Huna ubaguzi wa aina gani ya watu unaweza kukaa nao, popote unapokutana na watu unaweza kuanzisha mazungumzo na mkaenda vizuri.
7. Huogopi sana juu ya usalama wa ajira kwani unaamini hata bila ya ajira bado unaweza kuendesha maisha yako.
8. Mara kadhaa umekuwa ukigomea mamlaka. Umekuwa ukikataa maelekezo yanayotolewa na mamlaka kama hayaendani na misimamo yako ya ufanyaji kazi bora. Hii imekupelekea kuonekana ni mfanyakazi mkorofi na hata kufukuzwa.
9. Siku za mapumziko kama sikukuu au mwisho wa wiki ndio siku bora kwako kufanya kazi zako binafsi, huendekezi kupoteza muda kwa kupumzika au kustarehe.
10. Umewahi kuuza vitu vidogo vidogo ulipokuwa mtoto. Pia umewahi kufuga kuku, sungura na hata njiwa enzi za utoto wako.
11. Unapendelea kusimamia na kutoa maelekezo kwenye kampuni yako.
12. Una maono makubwa, unaona picha kubwa na tayari una mpango mkakati wa kufikia picha hiyo.
13. Unaona fursa kila mahali. Kwa mfano ukiwa sehemu yoyote mpya unajiuliza ni kitu gani cha uzalishaji kinaweza kufanyika eneo hilo na kunufaisha watu.
14. Mara nyingi unafikiria njia za kutatua matatizo ya watu na kuchukua hiyo kama fursa ya kibiashara.
15. Unafanya kazi zaidi ya masaa kumi kwa siku na sio chini ya siku sita kwa wiki. Muda mwingi unautumia kufanya kazi zako binafsi.
16. Unaweza kufanya kazi zako bila ya kusimamiwa au kuripoti kwa mtu mwingine. Husubiri upangiwe majukumu au ufatwe fatwe kuhakikisha unafanya kazi.
17. Chochote unachofanya unafikiria ni jinsi gani kitakupatia faida kutokana na muda na nguvu unazowekeza kwenye kitu hicho.
18. Unajali muda zaidi ya kitu kingine chochote. Kila mara unajiuliza kama unachofanya ni matumizi sahihi ya muda wako.
19. Watu wanakuona umeshanganyikiwa au hujui unachofanya. Kutokana na ufanyajikazi wako usio wa kawaida na malengo makubwa uliyonayo watu wengi wanafikiri umechanganyikiwa.
20. Unajua kwamba huwezi kufanya kila kitu mwenyewe hivyo kwenye kazi yoyote umekuwa ukijitahidi kutengeneza watu wengi zaidi wanaoweza kufanya kazi kwa ushirikiano mkubwa.
21. Uko tayari kubadilika haraka kutokana na mambo yanavyobadilika. Hung’ang’anii kufanya jambo kwa njia ambayo imeshapitwa na wakati.
22. Umejipanga na unajua jinsi ya kufanya yasiyowezekana yawezekane. Unaamini kila kitu kinawezekana iwapo utaamua kuwekeza muda na nguvu zako.
23. Unapendelea kufanya kazi kwa ushirikiano ila pia hutegemei uwepo wa wengine ili uweze kukamilisha majukumu yako.
24. Huendekezi usingizi. Unajua kupenda usingizi ni njia nzuri ya kuelekea kwenye umasikini, mara nyingi unalala kati ya masaa 6 mpaka 8 kwa siku.
25. Unapenda kufanya utafiti wa soko kabla hujatekeleza wazo lako kubwa la biashara. Unaelewa kwamba kuwa tu na wazo bora la biashara haimaanishi ndio kuwa na biashara yenye mafanikio, kuna vitu vingi vinahusika.
26. Unapenda kukaa na watu ambao wana mawazo chanya na wenye mipango mikubwa kwenye maisha yao. Kila unapokaa na wakatishaji tamaa na walalamikaji unajikuta unakosa raha na inakubidi uondoke.
27. Unaamini kwamba muda una thamani kubwa kuliko pesa, unaweza kupata pesa nyingi hata baada ya kupoteza, ila ukishapoteza muda huwezi kupata wa ziada.
28. Unafikiria nje ya boksi, na wakati mwingine unatoka kwenye boksi kabisa ili kupata picha ya tatizo na kuweza kutafuta njia ya kulitatua.
29. Umeacha chuo au umewahi kupata mawazo ya kuacha kuendelea na elimu baada ya kuona uhusiano wa elimu kubwa ya darasani na mafanikio ni mdogo sana.
30. Unapenda kujifunza mambo mapya kila siku. Unapenda kujisomea vitabu vya kujiendeleza binafsi na unatembelea mtandao wa internet kujifunza zaidi.
Kama una tabia hizo hapo juu na nyingine nyingi ambazo zinaendana na hizo tayari wewe ni mjasiriamali. Chukua hatua na kuanza kutumia uwezo mkubwa na vipaji ulivyonavyo ili uweze kufikia mafanikio makubwa.
Kama huna tabia hizo na unapenda kuwa mjasiriamali usikate tamaa, kwani jinsi muda unavyozidi kwenda utajikuta unafanya vitu hivyo kama umeshayaweka mawazo yako kijasiriamali zaidi.
Nakutakia kila la kheri kwenye harakati zako za maisha, TUKO PAMOJA.